Kizz Daniel ni mwimbaji na mtunzi wa nyimbo alizaliwa Mei 1, 1994 katika Jimbo la Ogun, mtaa wa Abeokuta Kaskazini na kupewa jina la Oluwatobiloba Daniel Anidugbe. Ana shahada ya ‘Water Resources Management and Agrometeorology (Water Engineering) aliyoipata katika Chuo Kikuu cha Kilimo Abeokuta mwaka 2013.
Akiwa katika mahojiano na Factory78 TV, Kizz Daniel alisema alianza kuimba akiwa na umri wa miaka saba na baba yake alikuwa akimuunga mkono kwa kiasi kikubwa na hata fedha ya kurekodi wimbo wake wa kwanza alimpa Naira100,000 wastani wa Sh560,000.
Soma pia Vanessa Mdee na Rotimi wanunua Jumba lingine Marekani
Mei 2015, alitoa wimbo wake wa tatu uitwao ‘Laye’ katika siku yake ya kuzaliwa, wiki chache baadaye aliachia video ya wimbo huo na Aje films, Mei 14, 2016 akaachia albamu yake ya kwanza, ‘New Era’.
Chini ya lebo yake, Fly Boy Inc, mwaka 2018 ulikuwa mzuri zaidi kwake alipomshirikisha Wizkid katika wimbo ‘For You’, kisha akampa shavu Davido kwenye ngoma ‘One Ticket’ iliyofanya vizuri.
Download Music: Rotimi – Love Somebody
Desemba 30, 2018 alitoa albamu yake ya pili ‘No Bad Songz’ ikiwa na nyimbo 20 ikiwemo ‘One Ticket’, aliowashirikisha wasanii kama Diamond Platnumz, Nasty C, Philkeyz, Demmie Vee, Dj Xclusive, Wretch 32, Diplo na Sarkodie.
‘No Bad Songz’, inatajwa kama albamu yake iliyofanya vizuri zaidi sokoni kwa kuongoza kwenye chati za iTunes nchini Marekani. Juni 25, 2020 aliachia albamu yake ya tatu ‘King of Love’ kisha ‘Barnabas’ (2021).
Mei 4, 2022 aliachia wimbo maarufu kwa sasa ‘Buga’ walioshirikiana na Tekno na video yake kutoka Juni 22, 2022 na kupata mapokezi makubwa kiasi cha kufikisha watazamaji milioni 40 YouTube ndani ya mwezi mmoja na kukaribia rekodi ya video ya wimbo ‘Jerusalema’ wake Master KG kutoka Afrika Kusini.
Hii ilifikisha watazamaji milioni 50 ndani ya mwezi mmoja na ndio video pekee ya muziki kutoka Kusini mwa Jangwa la Sahara iliyotazamwa zaidi YouTube hadi sasa.