Mwimbaji wa Country Music, Dolly Parton, 78, ameelezea furaha yake baada ya kupata habari kuwa huwenda wimbo wake maarufu, Jolene (1973) ukawepo katika Albamu mpya ya Beyonce.
Act II: Cowboy Carter itakuwa ni albamu ya nane ya Beyonce na imepangwa kuachiwa Machi 29, 2024 chini ya Parkwood Entertainment na Columbia Records.
Soma pia Afrika Kusini ilivyobadili mtazamo wa Alicia Keys
Akizungumza na Knox News hivi karibuni, Dolly Parton alijibu swali kuhusu uwezekano wa Beyonce kurekodi toleo lingine jipya la wimbo wake ‘Jolene’ uliovuma zaidi ya miaka 50 iliyopita.
Kwa mujibu wa Parton, huo ndio wimbo wake uliofanikiwa zaidi ambapo mwaka 2005 Jarida la Rolling Stone liliuweka namba 217 katika orodha ya nyimbo 500 bora duniani kwa muda wote, huku katika orodha ya mwaka 2021 ukiwekwa namba 63.
“Nadhani amerekodi ‘Jolene’ na nadhani labda utakuwepo kwenye albamu yake ya Country Music ambayo nimeifurahia sana kusikia ujio wake. Nampenda Beyonce, ni msichana mzuri na mwimbaji mzuri,” alisema Parton.
Hata hivyo, Parton alikiri kuwa bado hajafanikiwa kusikiliza wimbo mwenyewe licha ya kuwasiliana na Beyonce na mama yake mzazi, Tina Knowles ambao wote ni mashabiki wa muziki wake.
Parton alikuwa miongoni mwa wanachama wa mwanzo wa jumuiya ya Country Music waliojitokeza hadharani na kumpongeza Beyonce pindi alipotangaza ujio wa mradi huo unaongojewa na wengi kwa shauku kubwa.
Alifurahi sana pale wimbo wa Beyonce, Texas Hold ‘EM’ (2024) wenye mahadhi ya Country Music kushika namba moja katika chati za Billboard Hot Country Songs na kuandika rekodi kama mwanamuziki wa kwanza mweusi kufikia mafanikio hayo.
“Mimi ni shabiki mkubwa wa Beyonce na ninafurahi sana kwamba amefanya albamu ya Country. Hongera sana kwa wimbo wako wa kwanza kushika namba moja Billboard Hot Country. Siwezi kusubiri kusikiliza albamu kamili!,” aliandika Parton Instagram.
Download Music: Jux ft. Diamond Platnumz – Enjoy
Ikumbukwe Dolly Parton alivuma kimuziki na albamu yake ya kwanza, Hello, I’m Dolly (1967), hadi sasa ameuza rekodi zaidi milioni 100 duniani kote, ameshinda tuzo 11 za Grammy, huku utajiri wake ukikadiriwa na Forbes kufikia Dola440 milioni.